Habari rafiki yangu mpendwa,
hongera kwa kuendelea kujifunza kupitia Makala za uchambuzi wa vitabu ambazo
nimekuwa nashirikisha jamii kupitia mtandao wa FIKRA ZA KITAJIRI. Karibu katika
uchambuzi wa kitabu cha leo ambacho ni cha 8 kati ya vitabu 30 ambavyo nimejiwekea
lengo kuvisoma katika kipindi cha mwaka huu 2020.
Kama bado hujajiunga
na kundi letu la WhatsApp la FIKRA ZA KITAJIRI kwa ajili ya kupata neno la
tafakari kila siku pamoja na kujumuika na watu wenye mtazamo sawa, tafadhali JIUNGE
SASA.
Kitabu ninachokushirikisha
kupitia makala hii ni “The One Thing” kutoka kwa mwandishi Garry
Keller. Kupitia kitabu hiki mwandishi anatushirikisha mbinu mbalimbali kwa
ajili ya kuepuka kugusa gusa mambo mengi katika Maisha ili kuhakikisha kila
mara tunafanikisha jambo mojo baada ya jingine. Kuna msemo wa Warusi kuwa
“ukifukuza sungura wawili kwa wakati mmoja utajikuta umeshindwa kumkamata hata
mmoja wao”. Tafsiri yake ni kwamba, tunafanikiwa kimaisha pale tunapokuwa na utaratibu
wa kufanikisha jambo moja baada ya jingine.
Tunafanikiwa kwa
kuchagua kitu kimoja na kuhakikisha tunaweka jitihada kubwa za kuhakikisha kitu
hiko kinafanikishwa katika nyakati husika. Hivyo, mafanikio makubwa
yanapatikana kwa kuweka nguvu ya pamoja kwenye jambo moja kwa wakati husika.
Unapofanya mambo mengi kwa wakati mmoja unatawanya nguvu na rasilimali ambazo
zingetumika kufanikisha jambo moja kwa muda mfupi. Kutokana na mtawanyiko huo
wa nguvu na rasilimali, mara nyingi huwa ni mwanzo wa kukata tamaa kwa kuwa
hakuna tija kwenye yale unayofanya.
Watu wote tuna muda
sawa lakini tunatofautiana kimaendeleo, wapo wanaofanya kazi nyingi kwa
ufanisi, wapo wanaopata zaidi, wapo wanaingiza pesa nyingi na wapo wanaoangaika
kimaisha. Kama kipimo cha muda ni sawa kwa wote kwa nini pawepo tofauti hizo?
Mwandishi anatushirikisha kuwa wale wenye mafanikio katika Maisha wamejifunza
mbinu ya kufanya jambo moja baada ya jingine kwa wakati husika. Ni kupitia siri
hii, watu wenye mafanikio wanatekeleza majukumu yao kulingana na orodha ya
vipaumbele. Ni kupitia siri hii, watu wenye mafanikio wanatambua kuwa mafanikio
makubwa katika Maisha yanapatikana kwa kufanya vitu vichache kwa ufanisi
mkubwa. Kumbe, mafanikio yanapatikana kwa kufanya vitu vichache vyenye athari
chanya badala ya kufanya vitu vingi vyenye athari hasi.
Karibu ushirikiane nami kujifunza
machache kati ya mengi ambayo tunashirikishwa katika kitabu hiki:
UTANGULIZI
1.
Kulingana na gunduzi
za kisayansi, kitu kidogo katika mpangilio wa vitu vyenye mfanano wa mapana
hila urefu tofauti kina uwezo wa kusababisha mwendo ambao utaharibu utulivu wa
vitu vyote kwa mfuatano hadi kufikia kiwango cha mshindo mkubwa.
Kwa maneno rahisi ni kwamba, jambo dogo ambalo limetekelezwa kwa ufanisi lina
uwezo wa kusababisha matokeo makubwa katika Maisha. Ili ufanikishe matamanio au
ndoto ulizonazo ni lazima utambue ni ‘vitu vipi vidogo ambavyo utajitoa
kuvifanyia kazi kila siku kwa ajili ya ufanisi mkubwa katika kipindi cha muda
maalumu’. Mafanikio kwenye jambo dogo yanazaa mafanikio zaidi na kadri
unavyoendelea kufanikiwa ndivyo mafanikio yanaongezeka zaidi na zaidi.
2.
Makampuni na
biashara nyingi zinatambua umuhimu wa kujikita kwenye jambo moja, ndiyo maana
tunashuhudia kampuni zinazofahamika kwa kuzalisha aina moja ya bidhaa au kutoa
huduma moja kwa wateja. Kadri unavyojikita kwenye jambo moja ndivyo
unajitangaza kupitia jambo hilo na hatimaye kila mmoja atakufahamu, na hivyo
ndivyo mafanikio yanavyopatikana. Hivyo, ili ufanikiwe hauna budi kuchagua bidhaa
au huduma moja na kuhakikisha kila siku unatekeleza majukumu yanayolenga
kuiboresha bidhaa/huduma hiyo.
3.
Ili ufanikiwe
unatakiwa kutambua MTU MMOJA ambaye ndiye anashikiria mafanikio yako. Katika
historia ya Maisha yako fikiria mafanikio ambayo umewahi kupata kwa asilimia
kubwa yalichangiwa na nani? Jiulize ndoto/matamanio ya mafanikio katika Maisha
uliyonayo kwa sasa unahitakiji kupata mtu wa aina gani kwa ajili ya kufikia
matamanio/ndoto hazo. Hakuna mtu mwenye mafanikio ambaye amefikia mafanikio
hayo pasipo kushikwa mkono na watu wengine kwa namna moja au nyingine. Mtu huyo
mmoja anaweza kuwa mzazi, mwenza wako, rafiki, bosi, ndugu au mtu awaye yeyote
katika jamii kwa kuwa ulimwengu wa sasa umeunganishwa kuwa kitu kimoja. Hivyo,
tambua kuwa hakuna anayefanikiwa peke yake.
4.
Ili ufanikiwe
unatakiwa kutambua na kuendeleza KIPAJI au UJUZI maalum. Mwandishi
anatushirikisha kuwa mafanikio yanahusisha kutumia vipaji tulivyozaliwa navyo
au ujuzi ambao tunao kwa ajili ya kuzalisha bidhaa au kutoa huduma kwa jamii.
Watu wengi wanashindwa kufanikiwa kimaisha kwa kuwa wameshindwa kutambua ubora
wao upo wapi. Mafanikio yanakutaka ujitambue mwenyewe kwanza ikiwa ni pamoja na
kufahamu Maisha yako ni kwa ajili ya kufanikisha nini Duniani hapa.
SEHEMU
YA KWANZA: AINA ZA UONGO 6 AMBAO TUMEAMINISHWA KUWA KWELI
5.
Uongo #1: Kila kitu kina umuhimu sawa (everything matters equally). Usawa ni uongo ambao dunia imeubadilisha uonekane
kuwa ukweli. Katika hali yoyote chini ya maamuzi ya mwanadamu Duniani hakuna
usawa. Tulipokuwa Watoto tulijukuta katika hali ya utegemezi kwenye kila
tulichohitaji kufanya katika Maisha yetu. Kipaumbele namba moja katika umri huo
ilikuwa ni kucheza michezo ya kila aina na yeyote ambaye alikusudia kututoa kwenye
kipaumbele hicho kwetu alionekana mtu mbaya. Kadri miaka ilivyopita ndivyo
tulijikuta tunabadilika kutoka kwenye hali ya utegemezi na kuanza kutakiwa
kujitegemea wenyewe na pengine kuanza kutegemewa. Katika kipindi hiki cha
Maisha ya kujitegemea na kutegemewa ni lazima uwe tayari kufanya maamuzi
sahihi. Maisha yetu ni matokeo ya maamuzi tunayofanya kila siku kwenye kila
sekta. Katika kufanya maamuzi haya ndipo tunatakiwa kutambua kuwa hakuna usawa
Duniani, hivyo, chochote unachofanya hakikisha umeongozwa na mfumo wako wa
maamuzi.
6.
Watu wenye mafanikio
wana utaratibu wa kutekeleza majukumu yao kulingana na umuhimu na vipaumbele
vya majukumu husika. Hapa ndipo dhana ya kuwa “hakuna usawa Duniani”
unapotakiwa kuitumia katika majukumu yako kwa kuwa hata majukumu yetu ya kila
siku yana umuhimu na vipaumbele tofauti. Hata hivyo, ili ufanikiwe unatakiwa
kuwa na vipaumbele vyenye mwendelezo katika kila siku ya Maisha yako. Badala ya
kuandaa orodha ya majukumu ya siku unatakiwa kuondaa orodha ya vitu unavyohitaji
kufanikisha katika Maisha yako na kila siku kuhakikisha unapiga hatua kuelekea
kwenye ukamilisho wa orodha hiyo.
7.
Andaa vipaumbele vya
kutekeleza katika siku husika kulingana na tija yake katika kukamilisha orodha
ya vitu unavyohitaji kufanikisha. Kumbuka Duniani hakuna
usawa, vivyo hivyo, majukumu yako katika siku yana tija tofauti kwenye
uzalishaji wa matokeo. Hapa ndipo unatakiwa kuifahamu na kuitumia kanuni ya Vilfredo
Pareto mwanauchumi muitaliano ambaye katika karne ya 19 aligundua kuwa “takribani
asilimia 80 ya ardhi yote (au uchumi) ilikuwa mikononi mwa asilimia 20 pekee ya
idadi ya watu”. Baadaye kanuni iligundulika kuwa inafanya kazi katika
sehemu nyingi za Maisha. Mfano, asilimia ya 20 ya pembejeo inazalisha 80% ya
mazao; 20% pekee ya wafanyakazi wanazalisha 80% ya matokeo; 20% ya wateja
wanaleta 80% ya mapato na zaidi na zaidi. Kwa ujumla unatakiwa kupanga
vipaumbele vyako kulingana na tija ya uzalishaji wa matokeo kwenye orodha ya
vipaumbele vya mafanikio yako. Kumbe, ufanikiwe unatakiwa kujikita kwenye 20%
ya kazi ambazo zinaingiza pato la 80% ya matokeo yote. Asilimia 80 ya kazi
zinazobakia inabidi utafute watu wa kuifanya kwa ajili yako. Matokeo makubwa
(80) unayohitaji yanatokana na vitu vidogo (20) unavyovifanya kwenye majukumu
yako ya kila siku. Na pengine husiishie kwenye asilimilia 20 unaweza kutumia
kanuni hii kwa kupunguza vipaumbele kutoka asilimia 100 kuja 20 na kutoka
asilimia 20 kuja mpaka asilimia 1.
8.
Uongo #2: Kufanya kazi zaidi ya moja kwa wakati mmoja (Multitasking). Kufanya majukumu mawili kwa wakati mmoja ni uongo
kwa kuwa kati ya majukumu yote hakuna ambalo litafanyika kwa viwango
vinavyotakiwa. Maamuzi ya busara ni kukamilisha kazi moja baada ya nyingine. Hii
ni kutokana na ukweli kwamba, ubongo wa mwanadamu umeumbwa katika mfumo ambao
unawezesha kufanya kazi moja kwa ufasaha na siyo kufanya kazi zaidi ya moja kwa
wakati mmoja. Unaweza kuongea na kutembea au kunywa na kuandika lakini kutambua
kuwa matokeo yanayopatikana yanakuwa hayana au ubora ule ule ikilinganishwa
kama ungefanya kazi moja baada ya nyingine. Dunia ya sasa imejaa visumbufu
(distractions) vya kila aina ambavyo vinapoteza utulivu wa akili kwenye kazi
iliyopo mezani. Kuna usumbufu unaotokana na watu wa karibu yako (Ofisini au
nyumbani), milio ya simu kutoka kwenye simu janja, mitandao ya kijamii, barua
pepe na kila aina ya visumbufu ambavyo vinazuia ufanisi wa majukumu ya siku
husika. Ufanisi katika unapatikana kwa kutuliza akili kwenye jukumu moja baada
ya jingine.
9.
Ubongo wa mwanadamu
umesukwa katika hali ambayo inawezesha kufanya kazi zaidi ya moja japo katika
kazi hizo mhusika hawezi kutuliza akili kwenye kazi zote hizo.
Unaweza kusikiliza mziki huku unasoma au unaweza kutembea ukiwa unaongea lakini
kati ya vyote hivyo ni lazima ukubali moja lipate kipaumbele mbele ya jingine.
Unaweza kuweka utulivu wa akili kwenye matukio zaidi ya moja lakini tafsiri
yake ni kwamba akili umeigawa (divided mind) kushughulikia tukio zaidi ya moja
na matokeo yake ni ufanisi mdogo katika unayofanya. Kumbe pale tunapofanya
jambo zaidi ya moja ni lazima tuwe tayari kulipa gharama kwenye ufanisi/ubora
wa matokeo pamoja na muda au athari zinazoweza kujitokeza kama vile ajali. Kazi
ambayo ingefanyika kwa muda mfupi itatakiwa kufanyika kwa muda mrefu ili kupata
ubora unaohitajika. Watafiti wameonesha kuwa, takribani asilimia 28 ya muda wa
kazi katika siku unapotea kutokana na kukosa utulivu kwenye kazi moja. Tafiti
zinaonesha pia kuwa zaidi ya asilimia 16 ya ajali za barabarani zinatokana na
madereva au watumiaji wa barabara kushindwa kutuliza akili kwenye jambo moja.
10.
Uongo #3: Maisha yenye nidhamu. Kuna uongo uliogeuzwa kuwa ukweli kwamba mtu mwenye mafanikio ni lazima
awe na nidhamu. Huu ni uongo mwingine ambao tumeaminishwa. Ukweli ni kwamba
hatuhitaji nidhamu zaidi ya hii tuliyonayo ili kufikia mafanikio tunayotamani
bali tunatakiwa kuwa na mwongozo na usimamizi wa nidhamu tuliyonayo ili kufikia
mafanikio tunayotaka. Mafanikio siyo sawa na mbio za marathoni ambazo ukipoteza
nidhamu kidogo unaondolewa kwenye mbio na washindani wenzako. Mafanikio
yanahusisha utekelezaji wa yale ambayo huyatekelezi wakati unafahamu yana
mchango chanya katika kufikia matamanio yako. Hivyo, kwa lugha rahisi tunaweza
kusema kuwa mafanikio yanahusisha kujifunza tabia mpya na tabia hizo
zikishakuwa sehemu ya Maisha yako (daily routine) huna haja ya kuwa mtumwa
kupitia uongo wa nidhamu. Pointi muhimu ambayo mwandishi anatushirikisha ni
kwamba, “mafanikio yanapatikana kwa kufanya vitu vilivyo sahihi na siyo kufanya
kila kitu kwa usahihi (success is about doing the right thing and not about
doing everything right)”
11.
Tabia na nidhamu ni ambayo
watu wengi hawataki kuyasikia kutokana na ukweli kwamba yanaminya uhuru katika
Maisha. Maneno haya yanategemeana na pengine yametumika kumaanisha maana moja.
Ukweli ni kwamba katika Maisha unahitaji kuwa na nidhamu kwa ajili ya kujenga
tabia mpya. Hivyo, tabia zikishakuwa sehemu ya Maisha hazihitaji nguvu za ziada
kuendelea kuziishi. Baada ya kuwa na mkusanyiko wa tabia mpya ndipo mhusika
anaonekana kuwa mtu mwenye nidhamu (disciplined person). Kwa tafsiri hii,
hautaji kuwa na nidhamu ya kuishi vitendo vya kukuwezesha kufanikiwa bali
unatakiwa uwe na nidhamu ya kujifunza tabia mpya ambazo zinawezesha vitendo
hivyo kuwa sehemu ya Maisha. Tafiti zinaonesha kuwa inachukua angalau siku 66
mhusika kujenga tabia mpya. Na mhusika hawezi kujenga tabia mpya zaidi ya moja
kwa wakati mmoja. Na kadri mhusika anavyojenga tabia nyingi zenye kumwezesha
kufanya vitu nje ya mazoea yake ndivyo anaonekana mwenye mafanikio na nidhamu.
12.
Uongo #4: Nguvu ya utashi mara zote ni nguvu ya wito. Mwandishi anatushirikisha kuwa msemo wa “kwenye
utashi/nia mara zote kuna njia” umewapotosha watu wengi ikilinganishwa na jinsi
ulivyowasaidia. Msemo huu ukitafsiriwa katika upande mmoja unatoa nafasi kwa
mhusika kuwa na hamasa ya kufanikisha hitaji lake. Hata hivyo, msemo huu
unaacha kigezo cha umuhimu wa muda katika kufikia hitaji lako. Ukweli ni kwamba
ni vigumu kwa binadamu wa kawaida kuwa na nia/utashi wa kufanikisha hitaji lake
kila siku. Kuna siku ambazo anakuwa kwenye viwango vya juu vya utashi wa
kutekeleza kwa vitendo hitaji lake na zipo nyakati ambazo hajisikii kabisa
kujihusisha na lolote. Nguvu ya utashi kwa binadamu pamoja na kwamba inaweza
kuhuishwa (renewable) inapatikana kwa uchache (scarcity supply) kila siku.
Kutokana na ukweli huu, kama unahitaji kuwa na ufanisi mzuri huna budi
kuhakikisha nguvu hiyo inatumiwa kutekeleza vitu vya muhimu katika vipaumbele
vya siku husika.
13.
Tumeona kuwa nguvu
ya utashi inapatikana kwa uchache (limited supply).
Mfano, unapoamka asubuhi unakuwa na kiwango cha juu cha utashi wa kufanya kazi
na kadri muda unavyoenda ndivyo molali ya kazi inapungua. Kumbe, kama nguvu ya
utashi inapatikana kwa uchache (scarcity) kuna kila sababu ya kuhakikisha nguvu
hiyo inatumika ipasavyo. Kumbuka, tunapozungumzia nguvu ya utashi moja kwa moja
tunazungumzia uwezo wa akili au ubongo kustahimili kazi iliyopo mbele ya
mhusika. Ubongo wa mwanadamu ni takribani 1/50 ya uzito wa mwili wa mwanadamu
japo kiungo hiki kinatumia takribani 1/5 ya nishati yote mwilini. Na sehemu ya
ubongo yenye matumizi makubwa ya nishati ni ubongo wa mbele (prefrontal cortex)
ambayo inahusika na utulivu (focus), kutunza kumbukumbu za muda mfupi, kutatua
changamoto na kuhusika na uratibu wa vichocheo ambavyo mwili unatakiwa
kuitikia. Kumbe, ili sehemu hii ya ubongo iendelee kufanya kazi ni lazima iwe
na nishati ya kutosha kumwezesha mhusika kuwa katika kiwango cha juu cha utashi
wa kazi. Hivyo, ili sehemu hii ya ubongo iendelee kufanya kazi kwa ufasaha ni
lazima mhusika ajaze tenki lake la nishati kwa kutumia vyakula au vinjwaji
ambavyo vinahamsa kiwango cha sukari katika mzunguko wa damu.
14.
Kila siku pasipo
uelewa wetu tunajikuta kwenye kiwango cha chini cha utashi wa kazi pasipo kujua
kuwa sisi wenyewe ndo tumesababisha hali hiyo. Katika nyakati ambazo utashi wa
kufanya kazi upo kwenye kiwango cha juu tunatakiwa kutekeleza majukumu ya
vipaumbele vya muhimu ili kuepuka kupoteza nguvu ambayo ikipotea hairudi tena.
Kumbe, katika majukumu yetu ya kila siku tunapoteza nguvu ya utashi wa kufanya
kazi kutokana na sababu zifuatazo:-
รผ Kujaribu
kuishi tabia mpya katika majukumu yetu ya kila siku;
รผ Kuchuja
usumbufu unaojitokeza mara kwa mara;
รผ Kupambana
na vishawishi vinavyolenga kutuondoa kwenye vipaumbele;
รผ Kupambana
na hisia mbaya;
รผ Kujaribu
kuwaridhisha wengine;
รผ Kutatua
changamoto za mara kwa mara;
รผ Kupambana
na hofu;
รผ Aina
ya vyakula au vinywaji tunavyokula; au
รผ Kujihusisha
na kazi ambayo hauipendi kutoka rohoni.
15.
Uongo #6: Maisha ya mlinganyo (A balanced life). Hakuna
mlinganyo katika Maisha japo ni uongo ambao umeendelea kukubaliwa na wengi kuwa
ili ufanikiwe ni lazima uwe na mlinganyo katika Maisha. Maisha yanaundwa na
nguzo tatu ambazo ni: Kusudi, Maana na Faida. Ni lazima Maisha yawe na Kusudi
maalum, Maisha ni lazima yawe na Maana na Maisha ni lazima yawe na Faida kwa
mhusika pamoja na jamii inayomzunguka. Utatu huu hauwezi kuupata kwa kuishi
Maisha yenye mlinganyo kama ambavyo inaelezwa na watu wengi. Badala ya
kupambana kuishi Maisha ya mlinganyo unatakiwa kuishi Maisha yanayozingatia
kutekeleza vitu vya kipaumbele muhimu na si vinginevyo. Hii ni kutokana na
ukweli kwamba kadri unavyotumia muda mwingi kwenye majukumu ya kipaumbele
ndivyo inakuwa vigumu kuishi Maisha yenye mlinganyo kwa kuwa mambo yasiyo na
kipaumbele yananyimwa nafasi.
16.
Kuishi Maisha
mlinganyo maana yake ni kwamba uwe na uwezo wa kuwa katikatika ya Kazi
(majukumu) na Maisha ya kila siku. Maana yake ni kwamba
hautakiwi kujikita kwenye kazi zaidi na kusahau Maisha mengine nje ya kazi na
kinyume chake ni sahihi. Kama mlinganyo huu ungekuwa unawezekana ingekuwa ni
jambo lenye heri lakini ukweli kwamba Maisha ya kila siku yanatulazimisha kutoa
nafasi kwa baadhi ya vipaumbele na kuachana na mambo mengine kutokana na
uchache wa muda na rasilimali. Matokeo makubwa yanayoonekana kuwa muujiza
yanapatikana kwa kutekeleza majukumu ya kipaumbele na kuhakikisha kila mara
nguvu kubwa imewekwa kwenye maeneo hayo. Hata hivyo, mwandishi anatushirikisha
kuwa pamoja na kufanya kazi kwa kutekeleza majukumu ya kipaumbele tunatakiwa
kukumbuka umuhimu wa Maisha nje ya kazi.
17.
Muda haumsubirii mtu yeyote. Dunia imejaa watu wengi
ambao wanahairisha mambo kwa matarajio kuwa ipo siku watakuwa na muda wa
kuyarudia. Mfano, unaweza kupata muda wa kutekeleza majukumu yako ya kila siku
na kujikuta unakosa muda wa kukamilisha mahitaji muhimu katika Maisha binafsi.
Wafanyakazi au wafanyabiashara wengi wanakosa muda wa kuwa karibu na familia
zao kutokana na kubanwa na majukumu yao ya kazi. Mwandishi anatushirikisha
kuwa, muda haurudi nyuma wala haumsubiri mtu hivyo kadri unavyopata muda
hakikisha unatekeleza mahitaji yako muhimu katika Maisha. Tenga muda kwa ajili
ya kukamilisha vipaumbele vyako vya kazi, familia, masuala ya kijamii na
18.
Uongo #6: Kubwa ni baya (Big is bad). Huu
ni uongo mwingine ambao umezoeleka katika jamii. Ukweli ni kwamba “kikubwa
kinaweza kuwa kibaya na kibaya kinaweza kuwa kikubwa bila kusahau kuwa kidogo
pua kinaweza kuwa kibaya na kinyume chake ni sahihi”. Kutokana na uongo huo tumeaminishwa
kujikita kwenye hatua fupi fupi kwa kuogopa kuwa tukianza na hatua ndefu tutaanguka.
Fursa kubwa ni bora kuliko changamoto ndogo na changamoto kubwa ni mbaya kuliko
fursa ndogo. Hivyo, ukubwa hauna uhusiano wowote na ubaya maana uzuri au ubaya
unategemeana na hali ya tukio husika. Huu ni moja ya uongo kandamizi kwa kuwa
kama unaogopa mafanikio makubwa kwa kigezo kuwa mafanikio makubwa ni dhambi
(ubaya) kamwe hauwezi kupata mafanikio hayo.
19.
Watu wengi ni wahenga
(victim) wa kuogopa makubwa kwa kuwa kila panapotajwa matokeo makubwa watu wanayahusisha
na ubaya. Mfano, unapotaja neno utajiri kwenye kundi kubwa la watu, watu wengi
watakuambia mimi sitaki kuwa tajiri maana utajiri utanifanya nikose muda wa
kutosha kupumzika, matajiri ni watu wenye roho mbaya, utajiri utanifanya nikose
muda wa kutosha kuwa karibu na familia yangu; na mengine mengine. Unaweza kuona
ni jinsi gani uongo huu unaendelea kukandamiza Maisha yetu maana naamini hata
wewe mara nyingi umekuwa na hofu kila unafikiria kuanzisha hatua kubwa ambazo
zingezaa mafanikio makubwa. Kwa ujumla, kutokana na uongo huu tumekuwa waoga wa
matokeo/mafanikio makubwa. Kumbe, badala ya kuwa waoga wa matokeo makubwa kila
mara tunatakiwa kufikiria kutatua changamoto kubwa kuhusiana na malengo ya Maisha
yetu. Kila mara weka malengo yanayolenga kuongeza mara mbili thamani ya
mafanikio yako. Husiridhike na hatua unayofikia maana ili ufikie mafanikio makubwa
kila hatua inatakiwa kuwa chanzo cha kufungua hatua kadhaa mbele.
20.
Epuka ukanda wako wa
mazoea (comfort zone), epuka kufanya vitu kwa mazoea kama ambavyo kila mtu anafanya
(acting in a business as usual), fikiria tofauti, kuwa na fikra pana na tekeleza
majukumu yako kwa mapana. Hakuna mwenye kujua ukomo (limit)
wa uwezo wake katika kufikia mafanikio makubwa hivyo hakuna sababu ya kuwa na
fikra finyu ambazo zinaminya uwezo wetu halisi katika kila tunalofanya. Fikra pana
ni chachu ya kufikia mafanikio makubwa kutokana na ukweli kwamba mafanikio ni
vitendo na vitendo ni zao la fikra. Hivyo, mafanikio makubwa (big success) ni
zao la vitendo vya kishindo/tofauti (act big) ambapo ili utende tofauti ni
lazima uwe na fikra pana/tofauti (think big). Watu wote tumepewa muda sawa hila
kinachotofautisha mafanikio yetu ni yale tunayofanya katika muda huo.
Hii ni sehemu ya kwanza ya uchambuzi wa
kitabu hiki. Uchambuzi wa kitabu chote utapatikana kwa gharama ya Tshs.
10,000/=. Jiunge na mtandao wa Fikra za Kitajiri kwa KUBONYEZA HAPA.
Karibuni kwenye fikra za kitajiri ili upate
elimu isiyokuwa na mwisho.
Born to Win ~ Dream Big
Mwalimu Augustine Mathias
Namba ya Simu: +255 786 881 155
Mwanzilishi wa Mtandao wa fikrazakitajiri.blogspot.com
Barua pepe: fikrazatajiri@gmail.com